Mwalimu wa Shule ya Msingi Mitonji katika Kijiji cha Mitonji Kata ya Mbuyuni katika Wilaya ya Masasi mkoani Mtwara, John Mandanda amenusurika kuuawa na wananchi wenye hasira kali, baada ya kuwacharaza viboko wanafunzi hadi mmoja kupoteza fahamu. Mwanafunzi huyo wa darasa la sita (jina linahifadhiwa) anadaiwa kupoteza fahamu kwa zaidi ya saa moja. Kutokana na tishio la kuchapwa na wananchi hao walimu walimwokoa mwenzao kwa kumfungia ndani ya ofisi, huku wananchi hao waliotaka kumpa kichapo wakiwa wamebeba marungu, mashoka na silaa zingine za jadi. Akizungumza na Nipashe jana kwa njia ya simu, Ofisa Elimu Msingi Halmashauri ya Wilaya ya Masasi, Elizabeth Mlaponi, alisema mwalimu huyo alifanya tukio hilo juzi majira ya saa 5:00 asubuhi wakati wanafunzi walipokuwa wakiingia darasani baada ya mapumziko mafupi. Alisema mwalimu huyo akiwa shuleni hapo siku ya tukio, alitoa adhabu kwa baadhi ya wanafunzi ambao inaelezwa kuwa wanafunzi hao walikuwa wamechelewa kuingia darasani